NDOA NI KAMA YAI
Hongera nawapatia, bwana na bibi harusi
Kwa kufunga yenu ndoa, nawalaki kwa kikosi
Msojua mtajua, msende mwendo wa kasi
Hino ndoa kama yai, chungeni isivundike
Nawatakia salama, yenu yawe ni ya kheri
Muishi maisha mema, msikutwe nayo shari
Mzae watoto wema, wenye kumcha Qahari
Hino ndoa kama yai, chungeni isivundike
Indhari tukueni, muihifadhi moyoni
Yanayojiri nyumbani, ni siri yenu ya ndani
Yasipekwe kawandani kuwatia izarani
Hino ndoa kama yai, chungeni isivundike
Pamoja mshikaneni, na wala msiatane
Mazuri ambianeni, na mabaya mkanyane
Vicheko pia chekeni, maliwazo mpeane
Hino ndoa kama yai, chungeni isivundike
Kamba kwa shime vuteni, karipieni uvivu
Umoja udumisheni, ndipo mtapata nguvu
Maisha ulimwenguni, yahitaji ushupavu
Hino ndoa kama yai, chungeni isivundike
Matatizo kutokea, silo jambo la ajabu
Hayo yatawafikia, ingawa si matulubu
Kuelewana ndo ndia, ya kuimaliza tabu
Hino ndoa kama yai, chungeni isivundike
Vidudu watu wa tele, waipendayo zahama
Kwenu watapija lele, kuanzisha hiyo ngoma
Ikishazuka kelele, haraka watayoyoma
Hino ndoa kama yai, chungeni isivundike
Yao msiyasikize, hiyo ni yao ibada
Na wala msiyawaze, kwani hayana faida
Wacha waipige zeze, mwisho watakosa rada
Hino ndoa kama yai, chungeni isivundike
Kwa Mola elekeeni, ibada muidumishe
Radhi yake iyombeni, mema kwenu afikishe
Awaingize peponi, na moto awaepushe
Hino ndoa kama yai, chungeni isivundike
Annastecia Mbodze
Delete Comment
Are you sure that you want to delete this comment ?